Baada ya mshambuliaji wa Klabu ya Yanga Fiston Kalala Mayele kushindwa kufunga katika michezo minne,baadhi ya wazee waliojitambulisha kuwa wanachama wa Yanga wameeleza chanzo cha yote na namna ilivyokuwa.
Wazee hao ambao hawakutaka majina yao kuandikwa wamesema Mayele akiwa kwenye moja ya michezo ya ligi kuu,baada ya kumaliza mchezo alibadilishana jezi na mchezaji (hawakumtaja) wa timu pinzani Kisha mchezaji huyo kuondoka na hiyo jezi bila kuivaa na alikwenda kuiweka kwenye mfuko haraka haraka ikiwa bado na jasho na kuipeleka kwa mtaalamu waliekuwa nae kwenye gari siku ya mchezo huo.
Hata hivyo wazee wamesema wamefanya waliyoweza kufanya kurudisha uwezo wa Mayele kufunga na kuanzia mechi ijayo Mayele ataendelea kufunga kama kawaida
“Mchezo mzima tumeshaumaliza na kuanzia mechi ijayo Mayele ataendelea kutetema ila naomba kutoa tahadhari kwa yule aliyechukua jezi ya Mayele arudishe” Alisema Mzee mmoja kwa kujiamini.
Mzee mwingine alienda mbali zaidi na kusema kwa namna walivyofanya ana uhakika Mayele atafunga na kufikisha hadi mabao 20, Kisha akasema Mayele asipofunga mechi ijayo yuko tayari kuchoma kilinge.
